Miito



MWITO WA MUNGU KATIKA HISTORIA YA MWANADAMU

  1. Utangulizi

Mwanadamu hakuumbwa ili ajipe kila kitu au ajikamilishe yeye mwenyewe. Kuwa mwanadamu inamaanisha kuilekea hali iliyo juu yetu na kubwa kuliko ya kwetu. Hiyo hali ndiyo tunayoitafuta, au kwa lugha nzuri zaidi, huyo ndiye tunayemtafuta ili tukutane naye na kumpenda. Ili hali hiyo tuweze kuziishi ndipo hapo tunapokuja kujua  tunu mbili za maisha ya utawa: (i) kumwiga Kristo na (ii) kukutana na Mungu. Ili hilo liweze kuzaa matunda ni lazima kuwepo na wito.  

Sasa wito ni nini?

2. Wito
Neno wito linafanana na neno la kilatini «vocatio» likiwa na maana ya “mwito au mwaliko”. Hii nayo inatokana na kitenzi, «vocare», ikiwa na maana ya «ita». Ni mwelekeo wa ndani ya nafsi wa kupenda kitu fulani au maisha fulani. Roho inapoelekea. Hii inatafsiriwa kama sauti (vox) inayosikika ndani ya nafsi ya mtu. Ndipo hapo tunakutana na neno mwito au wito. Katika nyanja ya maisha ya kitawa tunasema: “mwanadamu ameitwa na Mungu kuishi maisha ya kitawa”. Kama sauti hii, mwelekeo huu umo ndani yetu, basi ina maana kuna aliyeuweka. Naye ni Mungu. Mungu ndiye anayeita. Mungu humwita mtu kwa jina (Is 45:3), mwito wake hauwezi kuujutia (Rum 11:29), kila mtu kaitwa peke yake (Yoh 21:22). Mwito wa Mungu ni kuitwa katika maisha kuingia maishani, ni mwito wa wokovu, ni mwito wa utakatifu, ni mwito wa kuingia katika muungano au usharika na Mungu. Hivyo wito ni kazi ya Mungu. Nao una sifa zifuatazo:
a)      Mwito ni fumbo. Chanzo chake ni Mungu.
b)      Kila mtu kaitwa kwa namna yake, (kivyake).
c)      Ni majadiliano ya upendo kati ya mtu na mwanadamu.
d)     Ni zawadi ya upendo.
e)      Ni Mungu anayejiweka karibu na mwanadamu.
f)       Ni kuongoka.
g)      Ni kufanya experience mpya ya maisha.
h)      Ni kuuelekea ukamilifu wa maisha.

3. Nifanyeje kuitikia mwito wa Mungu?
1.      Kitu cha kwanza ni kuona kuwa na uwezo wa kuyatafakari mambo yote yanayotokea na yanayogusa maisha yako mwenyewe. Jaribu kuingia katika ulimwengu wako wa ndani na kuona jinsi ulivyo na unavyoishi leo katika uhusiano wako na Mungu.
2.      Kitu cha pili uwe na uwezo wa kueleza hali yako ya ndani. Ndani mwako kuna nguvu zinazokuvuta kuelekea maisha yapi? Chukua diary yako ya kiroho jaribu kuandika matukio ya ndani. Unavutwa na maisha ya watakatifu? Unavutwa na maneno na maisha ya Yesu? Au unavutwa na nini?
3.      Jibidishe kusali sala binafsi. Sala zitakusaidia kufikia uamuzi muhimu na makini katika maisha yako na hivyo kutoa jibu sahihi. Sala inayokupeleka katika usikivu wa ndani.
4.      Jibidishe kujifahamu. Yasome maisha yako kwa makini. Unahisi kama Mungu ana mpango wowote na wewe? Una hofu?, ndani mwako una machafuko? Unatambua  udhaifu wako? Je hayo yote kwako yana maana gani? Ni kikwazo au ni faida?
5.      Jifungue kwa Mungu, kubali yanayotokea (Flp 2:5-7). Acha kile kitu unachokita hasa katika maisha kiwe wazi na tumaini ulimwengu uliobora zaidi. Kila siku acha sauti ya Mungu iongee ndani mwako. Sauti hiyo ilishe neno la Mungu kila siku.  Soma Biblia ili uweze kujua mapenzi ya Mungu. Kuwa mfano wa mtumishi. Achana na fahali za kidunia ambata na mtumishi mnyenyekevu Yesu Kristo.
6.      Hatua ya mwisho ni kuamua. Kinachoweza kukwamisha uamuzi ni hofu ya kukosea wito. Uamuzi unaangalia unachojifahamu leo. Unapima mahitaji ya wito na kuyajua yalivyo na kujipima leo. Maamuzi ya wito ni kuamini kuwa Mungu atakuongoza kwa maisha yako yote. Ni kuamini kuwa siku kwa siku anafanya kazi na kuishi pamoja na wewe na kuamini kuwa anaweza. Mfani ni wa Abramu, aliitwa akaenda pasipokujua alipokuwa anakwenda (Ebr 11:8). Jambo hili linatokana na swali la msingi, Mungu ni nani kwangu?
7.      Hitimisho. Ni kuacha yote na kumfuata Yesu Kristo. Swali litakuja. Naweza? Jibu tunalipata kutoka kwa Yesu anaposema. «Si ninyi mlionichagua mimi, bali ni mimi niliyewachagua ninyi; nami nikawaweka mwende mkazae matunda, na matunda yenu yapate kukaa» (Yoh 15:16).
8.      Inabidi uelewe kuwa katika wito huu, utamtumikia Mungu vizuri, utajitakatifuza na kutakatifuzwa na kupata wokovu, na utafanya kazi kwa ajili ya wokovu wa watu wengine nay a kuwa utamtukuza Mungu.  

4.0. Kukua katika wito
Kuishi kadiri ya tunu (values) za wito. Hapa kuna swali la msingi ambalo kila mmoja anatakiwa ajiulize. Nalo ni hili: Utafanyaje ili ukue katika wito wako na utatambuaje kuwa unakua? Hapa kinachoangaliwa ni uwepo wa tunu za wito na sababu zake. 

 4.1. Tabia. Kitu cha kwanza kinachoangaliwa na watu wengi ni tabia. Mfano, anasali, nimwema, ni mpole, ni mtii, anakaa vizuri na watu, anajua kufundisha vizuri dini. Kwa vipimo hivyo mara nyingi husema huyu atakuwa au Padre (Mtawa) mzuri au sisita mzuri. Na wanahitimisha kwa kusema kuwa ana wito. Hivyo kwa vigezo hivyo tabia inakuwa ni kielelezo cha tunu za wito. Kinachotakiwa ni kuzifanya tunu hizi ziwe na sababu ya ndani iliyo njema. Hivyo inabidi kujiuliza maswali haya: kwa nini unasali?,  kwa nini unatii?, kwa nini unapenda kukaa na watu?............n.k. unafanya hivyo kwa sababu ya tunu za wito au kwa sababu ya mahitaji yako mwenyewe ya kibinadamu?
Mfano kuna watu wanaonekana ni watii kwa kila kitu kumbe ni hofu ya kuogopa kuchukua majukumu mengine ya maisha. Unaweza kukaa na watu kwa ajili ya upendo na huduma lakini vile vile unaweza kukaa nao kwa kutafuta kusifiwa na kushukuriwa. Tabia ya nje ni nzuri lakini sababu ya ndani ni kinyume. Hivyo kinachoangaliwa ni kwa kiasi gani tunu hizo unazoziishi zitakuwa sehemu kweli ya maisha yako ya ndani ya wito wake. 

4.2 Tunu na kazi
Ili kutambua kuwa mtu anakua katika wito huangalia jinsi anavyopokea kazi na majukumu mengine. Hapa tunaangalia majukumu na nafasi wanayopewa watawa katika jamii. Majukumu haya humsaidia mtu kuzimwilisha tunu za wito na hivyo kukua, kutoka kwenye eneo la mahitaji binafsi na kuyafanya mahitaji ya kiwito. Inabidi kuwa makini sana na kazi tuzifanyazo. Mtu anaweza kufanya kazi nyingi sana na za kufaa, lakini akija katika sala, hasali. Hili ni jambo la hatari sana katika maisha ya kitawa. Hivyo neno kukua lina maana ya kuzibadilisha tunu zote na kuzifanya kuwa za kiwito. Hizo huonekana katika ishara tatu:
           i.     Kazi ni kielelezo cha tunu kama limechaguliwa si kwa kujifurahisha bali kwa ajili ya umuhimu wake. Kuwa na imani kuwa kitu hiki ni muhimu. 
         ii.     Kazi ni kielelezo cha tunu ikiwa aliyechagua kazi anafungamana nayo na kudumu katika huduma ya kitume bila kulalamika. Mfano kufundisha ni tunu, lakini pale mtu anapoifanya kazi ya kufundisha kama ndio msingi wa kuwa katika utawa, hapo kuna kuchanganya mambo. Mtu wa namna hiyo yuko tayari kuziweka pembeni nadhiri za kitawa. Kwake kikubwa si nadhiri bali kufundisha tu basi! Ikiwa ataambiwa aache kufundisha anajisikia kupoteza wito!
Mtu anayefanya kazi kwa tunu anakuwa huru ndani kufanya kazi yoyote.
       iii.     Na ya tatu ni pale ambapo kazi inafanywa kama njia ya maisha na si kama lengo la maisha. Kuna kazi ambazo humtaka mtu ajikatalie. Yesu anasema kujikana. Kama mtawa anaishi tunu hii, yuko tayari kwa lolote kulinda wito wake na tunu zake. Kinyume chake yuko hatarini kukata tamaa. Mwisho anaweza kuamua kuendelea na mtindo wake wa maisha na kufanya anavyoona yeye. Matokeo yake ni kufanya bila upendo. (1Kor 13:1-13). 

4.3 Mungu ana nia maalum nawe.

5. Miito katika Biblia.
Mungu anapomwita mtu, mtu huyo hubadilika kabisa. Hawezi kuishi kama alivyokuwa mwanzo. Kuitwa kwa mtu, ni kitu binafsi mno. Mungu alipomwita Ibrahimu hakuwaza au kufikiri, kilikuwa ni kitendo cha kipekee: «Bwana akamwambia Abramu, “Toka wewe katika nchi yako, na jamaa zako, na nyumba ya baba yako, uende mpaka nchi nitakayokuonesha”...(Mwa 12:1)». Abramu aliisikia sauti ya Mungu katika dhamira yake akafanya kama Mungu alivyomwagiza. Musa alikuwa anachunga kundi la mkwewe Mungu alipomwita kutoka kwenye kijiti cha moto (Kut 3:4). Mungu alimwita kijana Samweli, akimtaka kuwa tayari kupokea jukumu la kuibadili siasa ya utawala wa Israeli, (1Sam 3:1-21). Eliya alisikia sauti ya Mungu kwenye upepo mororo (1Fal 19:12-13). Kuna kipindi sauti ya Mungu inasikika hata kwenye keleke nyingi ikiwa anayeitwa atasikiliza kwa makini. Sauli (Paulo) (Mdo 9:1-4). 
 
3. Mt. Agostino
Alivyokuwa na akili na nia ya kumtafuta Mungu. Kwa sala za mama yake Monica alifanikiwa kumjua na kumpokea Kristo akabadilika kabisa katika maisha yake. 

4. Wito ni upendo wa Mungu unaojifungua ndani ya mwanadamu
Wito ni onesho la upendo Mungu unaopita vitu vyote na ambao huufanya moyo wa mwanadamu uwe wazi kwa ajili ya mambo ya Mungu. Mtu hubadilika na kuwa zawadi ya upendo kwa wengine na kwa maisha yake yote. Mwanadamu anayeitwa anaweza kukubali lakini vile vile yuko huru kuukataa huo upendo. Daima mwanadamu anapendwa na kuitwa na Mungu. Anachotakiwa kufanya ni kujiachilia mikononi mwake. Historia ya wito wa mwanadamu inaanzia kwenye uumbaji (Mwa 1-2) na itakamilika nyakati za mwisho ambapo kila kitu kitajumuishwa ndani ya Kristo (Efe 1:10). 

5. Uaminifu wa mwanadamu anayeitwa na Mungu
Mungu huonekana mwaminifu kwa Mungu anapoushinda ubinadamu wake. anayeonekana na mwaminifu ni yule anayetegemea kuyaweza yote kwa msaada wa Mungu. Ukweli huu, hujionesha jinsi anavyotenga muda wake kwa ajili ya kuongea na Mungu. 

6. Miito katika Agano la Kale-Wito wa Israeli na manabii
Tunapoongelea miito katika Agano la Kale, hasa tunalenga uhusiano wa kuteuliwa kwa upendo kwa taifa la Israeli. Kwa hiyo katika kuitwa kuna dhana nzima ya kuteuliwa, au kuchaguliwa. Mungu alifanya nao agano katika mlima Sinai ili wawe wajumbe wake kwa wengine. Ili kulidhibitisha hilo anawaita wazaliwa wa kwanza pale alipomtuma Musa awaokoe kutoka utumwani Misri, (Kut 4:22). Kati ya mataifa wao watakuwa ufalme wa makuhani, (Kut 19:6). 

6.1.  Majibu ya mwanadamu kwa Mungu
Mungu anapomwita mwanadamu huwa anasubiri majibu. Maneno yanayotumika kuonesha majibu yanayotakikana na haya: «isikilize sauti», «litunze agano la Mungu». Mfano taifa la Israeli linamjibu Mungu kwa kusema «Watu wote wakaitika pamoja wakasema, “Hayo yote aliyoyasema Bwana tutatenda”», (Kut 19:8a). Kilichowajenga kama taifa takatifu ni uhusiano mwema na Muumba wao, yaani, walitakiwa wajitenge na kila kitu ambacho hakiambatani na maisha ya kimungu. Hivyo wito halisi wa mwanadamu ni utakatifu. Mungu anamwita kila mwanadamu kuwa mtakatifu. Katika kuitikia wito wa utakatifu, huwa tunaitikia wito wa wokovu kwa kuishi ama maisha ya kitawa, ndoa, kipadri ama kuishi mwenyewe, lakini yote iwe ni kwa ajili ya ufalme wa Mungu. Ndipo hapo unakuta kila mtu anaitikia wito mkuu wa utakatifu kwa jinsi alivyoitwa kwa maisha mbalimbali. Mtume Paulo anasema: «Kila mtu na akae katika hali ileile ambayo alikuwa nayo alipoitwa» (1Kor 7:20). 

6.2. Wito wa manabii
Mungu alikuwa akiongea nao ndani ya dhamira zao. Tunapoangalia historia yao ya kuitwa tunaona karibia kila nabii aliweka kwanza ukinzani kabla ya kukubali. Hasa kilichowafanya kutokubali kirahisi ni kutambua udhaifu wao wa kibinadamu (Is 6:5), na kuhisi ugumu wa kufanikiwa katika misheni zao. walitambua kuwa kazi ya kinabii, mwisho wa siku haitawapa heshima yoyote mbele ya jamii, au faida binafsi, tena kinyume chake wataonekana kichekesho mbele ya jamii au adui! (Is 8:11-15), (Yer 15:10). 

4. Kutwa kwa Mitume
Yesu alipoanza kazi yake ya kuhubiri, alianza kuwaita watu mmoja mmoja ili wawe naye na wamfuate. Hawa ndio wale waliofahamika kama wanafunzi wake. Miongoni mwao alichagua kundi la watu kumi na wawili ambao ndio Mitume. Hawa ndio wale walioambatana naye katika kazi yake. Tukio la kuwachagua lilikuwa ni tukio kubwa kiasi kwamba kabla ya kulifanya alisali. Mwinjili Luka anasema hivi: “Ikawa siku zile aliondoka akaenda mlimani ili kuomba, akakesha usiku kucha katika kumwomba Mungu. Hata kulipokuwa mchana aliwaita wanafunzi wake; akachagua kumi na wawili miongoni mwao ambao aliwaita Mitume”. (Lk 6:12-13; Mk 3:13-19). 

5. Kwa nini Yesu aliwaita hawa Mitume?
Jibu tunalipata kutoka kwa Mwinjili Marko anaposema: “Akapanda mlimani, akawaita aliowataka mwenyewe; wakamwendea. Akawaweka watu kumi na wawili, wapate kuwa pamoja naye, na kwamba awatume kuhubiri, tena wawe na amri ya kutoa pepo”. (Mk 3:13-15). 

Aya mbalimbali za kuitwa katika Biblia.
Rum 8:29-30. Rum 9:11.
1Kor 1:4-9.
1The 2:12. 1The 5:24.
Gal 1:6.
Efe 1:18.
1Pt 1:15; 1Pt 2:9.
1Pt 5:10.

3. Kitu muhimu katika kuitwa kwao
Kwanza iliwabidi wakae naye, wamfahamu yeye binafsi na kufahamu kilichomleta ndipo hapo watumwe. Aliwaandaa ili wakalihubiri Neno. Hivyo walitakiwa watumwe, ndio maana wanaitwa Mitume. Yaani, waliotumwa. Ilibidi awaandae yeye mwenyewe na kuwapa mamlaka dhidi ya nguvu za mwovu. Haya ni mamlaka ya kimungu. (Mk 3:15).  

5. Umuhimu wa Mitume
Mitume walikuwa na kazi muhimu sana katika maisha ya Yesu. Mmoja wao, Yuda,  alimsaliti lakini wengine walibaki waaminifu kwa Yesu. Hawa ndio wale waliotoa ushuhuda juu ya yote aliyoyaisha na kuyafanya. Baada ya kifo na ufufuko wake Mitume walitiwa nguvu na Roho Mtakatifu wakaanza kuhubiri. Walieleza Yesu alikuwa nani na alifanya nini. Bila wao ujumbe wa Yesu usingesambaa duniani. Kuitwa kwao lilikuwa jambo kubwa na muhimu sana kwa ajili ya wokovu wa watu wengine.

6. Umuhimu wa kuitwa leo
Hata nyakati zetu, kuitwa ni kitu muhimu sana katika maisha. Mungu anaendelea kuwatumia watu wanaume kwa wanawake kuendeleza kazi ya Yesu iliyomleta duniani. Jambo hilo linategemea utayari wa nafsi ya mtu. Sauti ya Mungu inaita kutoka ndani mwa mtu ikimtaka aishi maisha fulani, kwetu sisi ni maisha ya utawa. Kuwa tayari kuacha yote kama Mitume na kuambatana na Yesu popote anakapotupeleka (Mk 10:28). 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Zingatia: Mwanachama wa blogu hii tu ndiye anayeweza kuchapisha maoni.

Home

Kundi la Wakarmeli Watanzania wa kwanza lililofungua misheni 2009 Bikira Maria na Nabii Eliya katika Karmeli