Skapulari ya Karmeli

Inatokana na neno la kilatini Scapulae ambalo maana yake ni mabega. Ni vazi refu ambalo linavaliwa juu ya kanzu ya kitawa. linaangukia mbele na nyuma. Hili ni vazi la kimonaki. Mfano Wabenedikitini, Wadominikani wanavaa Skapulari. Inasemekana Wabenedikitini ndio walioanza kuitumia kwenye karne ya 7 kama eproni. Matumizi yake yalibadilika na kuwa sehemu ya vazi rasmi la Shirika mbalimbali. Waliichukulia kama ishara ya mzigo mwepesi wa Yesu. Skapulari ni alama ya kuwa tayari kutumikia.


2. Aina za Skapulari 
Kuna aina mbalimbali za utengenezaji wa Skapulari. Kuna Skapulari yenye vipande viwili vya kitambaa cha brown chenye picha ya Bikira Maria wa Mlima Karmeli. Skapulari hii inapovaliwa kipande kimoja huangukia upande wa mbele yaani kwenye kifuani na kingine kinaangukia nyuma ya shingo yaani mgongoni. Skapulari hii inavaliwa na wale tu wanaojiweka wakfu kwa Bikira Maria wa Mlima Karmeli katika Utawa wa Tatu. Skapulari ndogo zenye kitambaa upande mmoja tu huvaliwa na wale wote wenye ibada kwa Bikira Maria wa Mlima Karmeli. Skapulari hii inaweza kuwa katika mfumo wa mwingine wa medali. Skapulari inavaliwa kwa ahadi maalum za kiroho. 

3. Maono ya Mt. Simon Stock na Skapulari ya Karmeli
Ibada kwa Skapulari –Historia, kukua na kusambaa kwa ibasa ya kiskapulari. Unapoongelea Ibada ya Skapulari unamaanisha Skapulari ya Bikira Maria wa Mlima Karmeli. Katika utamaduni wa maisha ya Wakarmeli, tunaelezwa kuwa Bikira Maria alimtokea Mt. Simon Stock huko Uingereza akamwambia kuwa wale wote wanaovaa Skapulari kwa uchaji wataokolewa moja kwa moja. Kipindi kile Shirika lilikuwa likipita kwenye kipindi kigumu cha mabadiliko (1247). Simon Stock –ambaye inaaminika kuwa ndiye aliyekuwa Mkuu wa Shirika, akawa anaomba msaada wa Bikira Maria. Alitaka kuona alama yoyote ya ulinzi wake wa karibu kwa Shirika. Mwishowe alitokewa na Bikira Maria akiwa na Skapulari mkononi mwake na kumwambia “Yeyote anayekufa amevaa Skapulari ataokolewa katika moto wa milele”.  


4. Bull “Upendeleo wa Jumamosi” 
Baadaye ulisambaa waraka mmoja (wa uongo) uliodaiwa kuandikwa na Papa Yohane XXII 03.03.1322. Katika Waraka huo (Sacratissimo uti culmine), Papa anasema kuwa alitokewa na Bikira Maria na kumwambia kuwa, Yeye Bikira Maria angewatoa Wakarmeli wote wanaovaa Skapulari kutoka Purgatori siku ya Jumamosi ya kwanza toka kufariki kwao kama watakuwa wamezingatia masharti ya: kusali Sala ya Kanisa, kuishi maisha ya usafi wa moyo, maisha ya sala na kuvaa Skapulari kila siku, wale wasio jua kusoma inawabidi kufunga siku zilizoamriwa na Kanisa. 

5. Wakuu wa Shirika katika juhudi za kuitambua Bull
Mkutano Mkuu wa Shirika wa uliofanyika mwaka 1517 uliagiza kuwa, juhudi zifanyike ili Hati hii “ya Kipapa” itambuliwe na Papa. Walimwomba Papa Leo X aitambue lakini alifariki kabla hajasema chochote. Baadaye Nicholas Audet alipewa Hati na Papa Klementi VII. Hati hiyo Ex clement ya 12.08.1530 ilihusu Bull ya Papa Yohane XXII, ilidhibitisha maombezi ya Bikira Maria kwa Wakarmel. Baada ya kupokea Hati hiyo Mkutano Mkuu ukatoa amri ya kuvaa Skapulari kwa ndugu wa Skapulari kwa manufaa ya kiroho. Yohane Mbatizaji Rossi alipata Hati Ut laudes kutoka kwa Papa Gregori XIII, 18.09.1577 iliyodhibitisha Rehema zilizotolewa na Mapapa waliomtangulia. Ilielezea upendeleo wa Bikira Maria kwa wale wanaovaa Skapulari. Hawa watapata ulinzi na msaada wake wa maombezi. Katiba za Shirika zilizochapishwa mwaka 1586 chini ya uongozi wa Yohane Mbatizaji Rossi ziliweka ibada ya kubariki Skapulari katika pontifikare ya kuvalishwa Skapulari. Mwaka 1604 Papa Klement VIII aliweka utaratibu wa kuwatambua ndugu wa Skapulari popote pale hata mahali ambapo Wakarmel walikuwa hawajafika. 

6. Mapapa na Skapulari
Papa Klementi VII, kwa Hati «Ex clementi Sedis Apostolicae» ya 12.08.1530 alidhibitisha Hati ya Upendeleo wa Jumamosi- Hati ya Jumamosi.
Papa Paulo III, kwa Hati «Provisionis nostrae», alidhibitisha upendeleo wa Jumamosi.
Papa Pio V, kwa Hati «Superna dispositione» alidhibitisha upendeleo wa Jumamosi, rehema na neema kwa Shirika la Wakarmel.
Papa Gregori XIII, Kwa Hati «Ut laudes» alidhibitisha rehema za upendeleo wa Jumamosi. Aliamuru Wakarmel wavae Skapulare muda wote usiku na mchana kwa ajili ya rehema ambazo watazipata na kwa kuokolewa watakapo kufa.
Papa Gregori XIV, alikuwa akivaa Skapulari kabla na baada ya kuwa Papa. Na alikuwa hali nyama siku ya Jumatano kulingana na utaratibu wa Shirika la Karmel.
Papa Leone XI, alikuwa akivaa Skapulari tangu mtoto. Alipochaguliwa kuwa Papa yule aliyekuwa akimvisha mavazi ya kipapa alitaka kuiondoa Skapulari. Lakini Papa alimkataza akisema kuwa huo uliokuwa ulinzi wa Bikira Maria. Alisema kuacha kuivaa Skapulari ni sawa sawa kumwacha Bikira Maria. Alisema “Niachie Maria ili Maria asiniache”.
Papa Paulo V, aliwahi kusema hivi: “Mapadri Wakarmel waruhusiwe kuhubiri kwamba, taifa la
Wakristo linaweza kwa uchaji kuamini juu ya msaada wa Bikira Maria wa Mlima Karmel kwa roho za kaka na dada walioishi naye: yaani, Bikira Maria atawasaidia kaka na dada wanaokufa katika upendo, ambao maishani walikuwa wakivaa Skapulari yake…, kwa maombezi yake ya daima, kwa sala zake za uchaji na mastahili yake, na kwa ulinzi maalum baada ya kufa na hasa siku ya Jumamosi. Kwa hiyo picha zinazotengenezwa au kuchorwa na wapenzi wa huyu Mama kwa njia yoyote ile hazimfanyi Bikira Maria ashuke kwenda toharani kwa ajili ya kuzifungulie roho, lakini roho hizi , kwa maombezi yake huchukuliwa mbinguni kutoka katika mateso yale kwa mkono wa malaika”.
Papa Alexander VII, Mwaka 1655, siku hiyo hiyo aliyotakiwa kuingia kwenye Koklave,
Alexander VII, Msiena aliyeitwa Fabio Chigi, alikwenda kwenye konventi ya Wakarmel wa Mt. Maria wa Transpontina, hapo baada ya kusali, alipokea kutoka kwa Pd. Mario Venturino, Mkuu wa Shirika (ndugu yake), Skapulari ya Maria na akaandikishwa katika kikundi cha ndugu wa Skapulari. Akiwa na alama hii ya ulinzi wa Mama wa Mungu, alielekea Vatikani na alichaguliwa kuwa Papa kwa msaada wa Bikira Maria (kama inavyoweza kuaminika), siku ya Jumatano, siku iliyotengwa na Wakarmel kwa ajili ya kumheshimu Bikira Maria Mama wa Mungu. Alikuwa na ibada maalum kwa Bikira Maria. 

7. Thamani na maana ya Skapulari
Anayepokea Skapulari huingizwa kiundani zaidi kwenye Shirika la Karmeli. Ni alama ya upendo na ujiwekaji wakfu kwa Bikira Maria ambaye ni Dada, Mama na mfano wa kila mfuasi wa Kristo. Anayeipokea hufanywa kuwa mwana familia ya Wakarmeli na hivyo hutakiwa kujibidisha kuishi maisha ya kiroho ya Wakarmeli. Kuishi katika urafiki wa ndani na Mungu kupitia undugu na maombi. Anayeivaa hukumbushwa kuishi maisha ya wakfu kwa Bikira Maria na hukumbushwa wajibu wa Shirika. Vile vile hupata ulinzi kutoka kwa Bikira Maria. Hutakiwa kuishi maisha ya sala, maombi, Alisema Papa Pio XII kuwa, Skapulari inaongea juu ya unyenyekevu, usafi wa moyo na fadhila zote za Maria ambazo inabidi tuzivae. 

Skapulari ni ishara au alama ya:
Kutumikia -kumfuata Yesu kama Maria, mfano kamili wa wafuasi wote wa Kristo. Chimbuko la wajibu huo uko katika Ubatizo unaotufanya watoto wa Mungu. Maria anatufundisha jambo hilo.
Kuishi maisha yanayojifungua kwa Mungu na kwa kufuata mapenzi yake yanayojionesha katika maisha.
Kusikiliza Neno la Mungu katika Biblia na katika maisha, kuliamini na kuweka katika matendo matakwa yake.
Kusali daima na kutambua uwepo wa Mungu katika matukio yote.
Kuwa karibu na ndugu zetu wanaoishi katika matatizo mbalimbali.
Kutuonesha mfano wa watakatifu Wakarmeli.
Kulinda roho zetu zisichafuke

Imani ya kukutana na Mungu katika maisha ya milele kwa maombezi ya Bikira Maria. 

8. Ndugu Wakarmel
Hapo zamani kulikuwepo vikundi mbalimbali vya walei katika Shirika la Karmel. Hawa waliitwa ndugu Wakarmel. Vikundi vikubwa vilikuwa viwili:

1. Ndugu wa joho jeupe
Kundi hili la walei waliokuwa wakivaa vazi joho jeupe la Shirika (Mantello bianco) lilikuwepo hata kabla ya kundi la Ndugu wa Skapulari. Walikuwa ni utawa wa tatu. Kazi yao ilikuwa ni kueneza ibada kwa Bikira Maria kwa kuandaa maandamano wakati wa sherehe za Bikira Maria. Walikuwa wakiungana kusali na kuimba nyimbo za Bikira Maria. Walijishughulisha kutoa michango kwa ajili ya kutunza maeneo ya Bikira Maria. Vaza lao lilikuwa ni joho jeupe. 

2. Ndugu wa Skapulari:
Ni kundi la waamini walei wanaojibidisha kuishi maisha ya ukamilifu wa upendo duniani katika roho ya Shirika la Wakarmel.  Kujitoa kwao kwa uhuru wanashiriki maisha ya Shirika na kupata manufaa ya kiroho katika muungano wa ndani wa mawazo, mipango na kazi wakiwa pamoja  na Maria. Mwenye Mamlaka ya kuwaweka kisheria katika Shirika ni Mkuu wa Shirika. Ruhusu inayotolewa na Askofu ya kuweka nyumba ya kitawa katika jimbo lake inaendana na ruhusa ya kuweka kikundi cha ndugu wa Skapulari. Lakini mahali pengine pasipokuwa na nyumba au konventi, inahitajika barua ya ruhusa kutoka kwa Askofu. Wanatakiwa kupokelewa katika Shirika na mtu mwenye mamlaka ya kufanya hivyo kwa jina la Shirika. Kupokelewa hufanyika kwa mujibu wa taratibu za ibada zilizowekwa na Vatikani. Lazima kujiandikisha kwenye kikundi na baadaye hupokelewa kwa kuvalishwa Skapulari. Jina lake linaandikwa katika kitabu cha kumbukumbu likiwa na tarehe yake ya kupokelewa. Inawabidi kuvaa Skapulari muda wote kuonesha kushiriki katika Shirika la Wakarmel. Lakini zaidi kushiriki sala, kushiriki Ekaristi Takatifu na kusali kila siku Sala ya Kanisa na kusali rozari kila siku. Sikukuu yao huadhimishwa tarehe 16 Julai.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Zingatia: Mwanachama wa blogu hii tu ndiye anayeweza kuchapisha maoni.

Home

Kundi la Wakarmeli Watanzania wa kwanza lililofungua misheni 2009 Bikira Maria na Nabii Eliya katika Karmeli